Thursday, November 3, 2016

Kenya yatangaza kuondoa wanajeshi Sudan Kusini

Kenya imetangaza kuwa inawaondoa wanajeshi wake kutoka kikosi maalumu cha Umoja wa Mataifa cha kudumisha amani kilichoko Sudan Kusini, baada ya kamanda wake kutimuliwa kazini.
Wizara ya Mashauri ya Kigeni imesema kuwa utaratibu wa kumuachisha kazi Jemedari Johnson Mogoa Kimani Ondieki haukuwa na uwazi.

Katibu Mkuu wa UN Ban Ki-moon alimfuta kazi Luteni Kanali Johnson Ondieki baada ya ripoti ya uchunguzi kusema alikosa kuwajibika kulinda raia mapigano yalipozuka upya nchini Sudan Kusini mwezi Julai.
Ripoti hiyo imesema walinda amani waliokuwa chini ya jemedari huyo hawakuchukua hatua yoyote wanajeshi wa serikali waliposhambulia kituo cha utoaji misaada mjini Juba na kuwadhulumu raia.
Kenya imesema uamuzi huo si wa haki na kutangaza kwamba itayaondoa mara moja majeshi yake yanayohudumu chini ya UN nchini Sudan.
Kadhalika, Kenya imejiondoa kutoka kwa mpango wa kutuma wanajeshi wa ziada kutoka nchi za kanda ambao walitarajiwa kutumwa kuimarisha kikosi cha UN nchini humo.
Kwenye taarifa yake, Kenya imesema kwa kumfuta Jenerali Gen Ondieki, Bw Ban alikosa kuangazia kiini cha matatizo yaliyobainika kwenye ripoti hiyo ya uchunguzi.

Habari kwa hisani ya bbcswahili.com


No comments:

Post a Comment