Friday, June 21, 2013

Mabondia wa Tanzania wafungwa Mauritius

Mabondia waliohukumiwa


Mabondia wanne wa Tanzania wafungwa miaka 15 jela nchini Mauritius kwa makosa ya kuingiza dawa za kulevya aina ya heroin.

Mabondia hao ni Case Ramadhani Fills, Nathanael Elia Charles, Ally Rajabu Msengwa na Petro Charles Mtagwa.
Wakiwa mbele ya Jaji, waliiambia mahakama kuwa walilazimika kuingia katika biashara hiyo haramu kutokana na hali zao za maisha kuwa maskini.Wakati kesi hiyo ilipoanza kusikilizwa, wote walikiri makosa ya kuingiza mihadarati hiyo nchini Mauritius wakati walipokwenda kushiriki mashindano ya ndondi barani Afrika mwaka 2008.
"Tunaomba radhi kwa taifa la Mauritius", waliiambia mahakama.
"Tu watu maskini na tunategemewa na familia, watoto na wazee wetu wanatutegemea."
"Kwa dawa hizi tungepata kiasi cha Pauni £4,000". walisema
Jaji Benjamin Marie Joseph alisema katika kutoa adhabu hiyo yote hayo ameyafikiria, kwani walitoa ushirikiano mzuri wakati wote wa uchunguzi wa kesi hiyo, kulikowezesha hata wafanyabiashara hiyo, raia wa Mauritius kukamatwa.
Wamekuwa mahabusu kwa siku 1,722, sawa na miaka mitano, hivyo watatumikia miaka kumi iliyobakia jela. Pia watatakiwa kulipa faini ya pauni £1,600 na gharama nyingine za uendeshaji wa kesi hiyo.
Kwa mujibu chanzo cha habari nchini Mauritius, Jaji aliwashutumu kwa kuukosea umma wa Mauritius kwa kuingiza dawa hizo za kulevya aina ya heroin.
Mabondia hao waliwasili Mauritius tarehe 10 Juni 2008 na kuweza kupita uwanja wa ndege bila kunaswa hadi walipokamatwa katika hoteli waliyofikia ya Quatre Bornes.
Kwa pamoja walimeza gram 4639.04 za heroin zikiwa katika vifuko 358 vijulikavyo kama pipi.

No comments:

Post a Comment