Monday, June 24, 2013

Mshtakiwa wa EPA asimulia jinsi wajanja walivyomzidi ‘kete’ kwenye akaunti yake

Mkurugenzi wa Kampuni ya Principal Ltd, Godfrey Mosha amesimulia jinsi Benki ya Akiba Commercial (DCB), tawi la Kariakoo, ilivyoidhinisha malipo ya fedha kwa mtu mwingine kutoka akaunti yake ndani bila yeye kujua.
Mosha ni mmoja wa washtakiwa katika kesi ya  wizi wa fedha kwenye  Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Pamoja na wenzake, Bahati  Mahenge, Manase Makale, Davis Kamungu na Eda Makale, wanakabiliwa na kesi ya wizi wa Sh1.86 bilioni za EPA, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kuipitia Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex.
Katika kesi hiyo dhidi ya DCB, inayosikilizwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Warialwande Lema, Mosha anaidai benki hiyo Sh46.8 milioni, zilizolipwa kwa mtu asiyemfahamu kwa kutumia hundi nne tofauti na tarehe tofautitofauti.
Katika ushahidi wake Ijumaa  iliyopita, akiongozwa na Wakili wake, Michael Ngalo, Mosha alidai  alibaini uhamisho huo wa fedha  kutoka  akaunti yake namba 0400438671, Novemba 15, 2011 alipochukua taarifa ya benki.
Alidai kuwa baada ya kubaini uhamisho huo, alikwenda makao makuu ya benki hiyo ambako alimuona Meneja wa Fedha, Vicent Anthony na kumweleza kuhusu tukio hilo wakati yeye hajawahi kuidhinisha uhamisho huo.
“Vicent aliniambia kuwa siyo transfer (uhamisho), bali ni malipo yaliyofanyika kwa kutumia cheque (hundi). Aliniambia namba za hundi hizo na ikaonekana kuwa zililipwa kwa Rafael John Mkwabi, mwenye namba ya akaunti 11000787541,” alidai Mosha na kuongeza:
“Huyo John sijawahi kumwandikia hundi, wala sijawahi kufanya naye biashara, sijawahi kukutanana naye, wala simfahamu.”
Mosha alidai kuwa hundi hizo zilikuwa zimesainiwa na Vicent na Meneja Mkuu, Salehe Ramadhan, huku akidai kuwa saini inayoonekana katika hundi hizo siyo yake.
Alizitaja hundi hizo kuwa ni hundi namba 083722, ya Sh11.6 milioni iliyolipwa Novemba 11, 2011 na  hundi namba 083723 ya Sh9 milioni, iliyolipwa tarehe hiyo.
Nyingine ni  hundi namba 083724 ya Sh14.4 milioni iliyolipwa Desemba 2011, hundi namba 083725 ya Sh11.8 milioni iliyolipwa Desemba 3, 2011.
Aliziwasilisha mahakamani hundi hizo na nyaraka mbalimbali zinazoonyesha saini yake halisi, mahakama ilizipokea kama vielelezo vya ushahidi.
Baada ya kumaliza kutoa ushahidi wake, Wakili Ngalo alifunga ushahidi na mahakama ilipanga kuendelea na usikilizaji kesi hiyo Julai 8, wadaiwa wataanza kujitetea.

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment