Viongozi wanne wa vyama vya upinzani mkoani Mtwara,
wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, wakikabiliwa na
mashtaka matatu ikiwamo kula njama, kufanya uchochezi na kuamsha hisia
mbaya kwa wakazi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Washtakiwa hao ni Katani Ahmed Katani (33) na
Saidi Kulaga (45) wa CUF, Hassan Uledi (35) wa NCCR Mageuzi, Hamza
Licheta (51) wa TLP, wote wakazi wa Mtwara.
Awali Katani, Uledi na Licheta walifikishwa
mahakamani Mei 31 mbele ya Hakimu Mfawidhi Mwandamizi, Dainess Lyimo,
kabla ya kuunganishwa na Kulaga ambaye alikamatwa Juni 2 mwaka huu na
kufikishwa mahakamani peke yake Juni 3.
Hata hivyo, juzi washtakiwa wote wanne
waliunganishwa na kufikishwa kwa Hakimu Mkazi Mussa Esanju, kutokana na
kile kilichoelezwa kuwa Hakimu Lyimo yupo safarini.
Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Justine Sanga,
alidai washtakiwa hao kwa pamoja walikutana mahali na muda usiojulikana
na kula njama hizo.
Sanga alidai shtaka la pili, Januari 16, mwaka huu
eneo la Bima mjini Mtwara, washtakiwa kwa pamoja walidaiwa kufanya
makosa ya uchochezi, kwa kutoa hotuba kwa wakazi hao, kwa lengo la
kuleta chuki na kusababisha kuharibu mali za umma na binafsi.
Pia, alidai shtaka la tatu Januari 16, mwaka huu
eneo la Bima washtakiwa kwa pamoja wanadaiwa kuamsha hisia mbaya,
kufanya mikutano ya kisiasa, kutoa maneno makali na kusababisha kuamsha
hisia mbaya za wananchi.
Wakili wa utetezi, Banana Biboze aliomba mahakama
kumwachia mteja wake, Hassan Uledi, ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu
cha Waislamu Morogoro (Mum) kwa ajili ya maandalizi ya mitihani yake
Juni 16, mwaka huu.
Hata hivyo, mahakama haitoa dhamana kwa washtakiwa
hao kwa kile kilichodaiwa ni kwa ajili ya usalama wa washtakiwa na
jamii na kwamba, Hakimu Lyimo anayesikiliza kesi hiyo yupo safarini.
Washtakiwa kwa pamoja walikana mashtaka na kurudishwa rumande hadi Juni 13, mwaka huu.
Source:Mwananchi
Source:Mwananchi
No comments:
Post a Comment