Monday, April 15, 2013

JK awaonya viongozi wanaoleta mvutano kuhusu barabara

Rais Jakaya Kikwete amewaonya viongozi wanaoleta mvutano juu ya wapi ipitishwe Barabara ya Tanga-Pangani-Saadani hadi Bagamoyo kwa kuwa wanaendesha ubishani unaoweza kuwachanganya wataalamu walioshughulikia suala hilo.
0are
Mkinga. Rais Jakaya Kikwete amewaonya viongozi wanaoleta mvutano juu ya wapi ipitishwe Barabara ya Tanga-Pangani-Saadani hadi Bagamoyo kwa kuwa wanaendesha ubishani unaoweza kuwachanganya wataalamu walioshughulikia suala hilo.
Amesema baada ya kumalizika kwa barabara ya Tanga-Horohoro,Serikali yake sasa kwa Mkoa wa Tanga itaelekeza nguvu zake katika ujenzi wa Barabara ya Tanga-Pangani-Saadani hadi Bagamoyo.
Alisema hayo juzi alipokuwa akifungua barabara mpya ya kiwango cha lami ya Tanga-Horohoro katika sherehe zilizofanyika kwenye kituo kipya cha mabasi cha Wilaya ya Mkinga kilichopo Kasera wilayani hapa.
Barabara hiyo ya Tanga- Horohoro ya urefu wa kilometa 65 imejengwa na Kampuni ya kutoka China ya Sinohydro Corporation Ltd iliyokabidhiwa rasmi kazi hiyo Januari 4, mwaka 2010 baada ya kuingia mkataba baina yake na mfadhili ambaye ni mfuko wa Millenium Challenge (MCC) na Serikali ya Tanzania kwa gharama ya Sh69.8 bilioni. Akizungumza katika sherehe hizo zilizohudhuriwa na mabalozi wa kutoka nchi za Marekani, India, Kenya, watendaji wakuu wa MCC, mawaziri, wakuu wa mikoa ya Tanga, Pwani na wananchi, Rais Kikwete aliwaonya wanaoleta mvutano juu ya barabara hiyo kwamba wanawavuruga wataalamu.
Alikuwa akizungumzia juu ya mvutano uliojitokeza kuhusu wapi ipite barabara hiyo, ambapo wapo wanaokubaliana na wataalamu wanaotaka ipitie ndani ya Hifadhi ya Mbuga ya Taifa ya Saadani huku wengine wakiwamo wanamazingira wakipinga kwa madai kwamba ikipitishwa katikati itawafukuza wanyama waliomo.
Hotuba hiyo ya Rais Kikwete ni majibu kwa kamati ya ushauri mkoa wa Tanga ambayo katika kikao chake kilichofanyika mwezi uliopita ulijitokeza mvutano wa wapi ipitishwe barabara huku wajumbe wengine wakitaka ipite katikati ya hifadhi na wengine wakihadharisha kuwa itaathiri ustawi wa wanyama.
Katika kikao hicho kilichofanyika chini ya uenyekiti wa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Gallawa, wajumbe waliagiza iandikwe barua kwa Rais Jakaya Kikwete kumuomba kukubali pendekezo la kupitisha barabara nje ya hifadhi.
Barabara hiyo kama itapitishwa katika hifadhi ya Saadani itakuwa ya urefu wa kilomita 175 na ikiwa itazungushwa na kupitishwa nje ya hifadhi italazimika kuongezeka urefu wa kilomita 35 nyingine ambapo kwa sasa ipo kwenye hatua ya kufanyiwa usanifu.
Barabara hii ya Bagamoyo-Saadan-Pangani –Tanga itajengwa kwa ushirikiano wa nchi za Jumiya ya Afrika Mashariki,ambapo kwa upande wa Kenya mradi huu unahusisha ujenzi wa barabara ya Horohoro-Lungalunga-Mombasa hadi Malindi.

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment