Friday, May 3, 2013

KUFA AZIMIO LA ARUSHA:Nyerere alivyotofautiana na Mwinyi

Kumekuwa na mjadala kuhusu sababu za kufa kwa Azmio la Arusha. Azimio hilo lilianzishwa na Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama cha Tanu kikiwa na lengo la kutilia mkazo imani na siasa yake ya Ujamaa na Kujitegemea.
Halmashauri hiyo iliyokutana mjini Arusha Januari 26 - 29, 1967, ilijadili maadili ya viongozi wa umma, Serikali na vyombo vingine, pamoja na wanachama wa Tanu.
Katika maadili ya viongozi wa umma, iliamuliwa kuwa kiongozi wa Tanu (baadaye CCM) au wa Serikali, sharti awe ama mkulima au mfanyakazi na asishiriki katika jambo lolote la kibepari au kikabaila.
Hata hivyo baada ya Mwalimu Julius Nyerere aliyekuwa anasimamia maadili hayo kung’atuka madarakani, misimamo hiyo ilianza kuyeyuka na kupigiliwa msumari wa mwisho huko Zanzibar.
Maamuzi ya Zanzibar
Mwaka 1991 Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi  (CCM) ilikutana mjini Zanzibar na kufanya mabadiliko ya azimio hilo.
Akizungumza na wazee wa chama, viongozi wa Taifa, mashirika ya umma na watu binafsi Februari 25, 1991 jijini Dar es Salaam, aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM  hicho na Rais Ally Hassan Mwinyi aliwatoa hofu wale wanaodhani kuwa azio la Arusha linageuzwa.
“Inaelekea kuna hofu kwamba Azimio la Arusha linageuzwa. Kwa hiyo tangu mwanzo, kabla ya kusema lolote, nataka tuelewane kwamba siasa yetu bado ni ile ile ya Ujamaa na Kujitegemea,” anasema na kuongeza:
“Halikugeuka wala hatutazamamii kuligeuza. Kwa hali yoyote sisi wanachama wa Chama cha Mapinduzi hatutaweza kuigeuza siasa hii. Kule Zanzibar tulizungumza mengi, miongoni mwao ni kutoa tafsiri ya baadhi ya vipengele vya Azimio ili vifanane na wakati tulionao.”
Akifafanua zaidi, Mwinyi anasema tangu azimio hilo lilipoanzishwa mwaka 1967 hadi mwaka 1991 ilikuwa imepita zaidi ya miaka 20, hivyo kulikuwa na mabadiliko mengi duniani.
“Hali yetu ya sasa hasa ya kiuchumi, siyo ile ya mwaka 1967. Ndiyo maana mishahara ya wafanyakazi ingawa imeongezeka sana, lakini bado haikidhi mahitaji yao, haiwatoshi hata wale wanaopokea mishahara mikubwa miongoni mwetu,” anasema na kuongeza:
“Isitoshe, wakati wa Azimio idadi ya Watanzania ilikuwa ndogo, sasa hivi idadi yetu imeongezeka zaidi ya mara mbili . Kwa sababu ya wingi wetu, mahitaji yameongezeka sana, wakati mapato yetu yamekuwa yakipungua wakati wote.”
Mwinyi anaongeza kuwa kila zama na mwongozo wake:
“Msahafu wa Waislamu unasema “Likulli ajalin kitab’, yaani kila zama ina kitabu chake,” anasema na kuongeza:
“Sisi wana CCM tunakubali kuwa kila zama zinahitaji kuwa na mwongozo wake. Azimio la Arusha ni mwongozo wetu wa msingi. Ni dira inayoongoza mwelekeo wa jamii yetu. Lakini tafsiri zake inabidi zirekebishwe kila inapohitajika ili zisipitwe na wakati.”
Akisisitiza kuhusu ufafanuzi wa maamuzi ya Zanzibar anasema baada ya kutangazwa kwa azimio la Arusha mwaka 1967 lilifuatiwa na matamko kama vile Azimio la Iringa la mwaka 1971 la ‘Siasa ni Kilimo’ na mwongozo wa mwaka 1981 uliotolewa kwa lengo la kukuza tafsiri ya Azimio la Arusha.
Anaongeza kuwa hata mwaka 1974 kulikuwa na agizo la Musoma kuhusu Elimu ya Kujitegemea.
“Maandiko hayo yote hayakupingana na Azimio la Arusha, ila yaliongeza mambo ambayo yalihitajika yafanane na wakati wake,” anasema.
Akizungumzia sababu ya kuanzishwa kwa Azimio la Arusha mara baada ya nchi kupata uhuru, anasema baadhi ya viongozi walianza kutumia uongozi wao kama mradi wa kujineemesha.
Msimamo wa Nyerere
Licha ya Rais wa awamu ya pili kufafanua umuhimu wa uamuzi wa Zanzibar, bado Mwalimu Nyerere aliendelea kutoridhika kuhusu msimamo mpya wa CCM.
Akizungumza na waandishi wa habari mwaka 1999, Mwalimu Nyerere alisema bado alikuwa hajaona kasoro ya Azimio la Arusha. “Mimi bado natembea nalo (Azimio la Arusha). Nalisoma tena na tena kugundua kama kuna cha kubadili. Labda ningeboresha Kiswahili nilichokitumia, lakini Azimio lenyewe bado ni thabiti. Nisingebadili hata neno moja,” anasema Mwalimu Nyerere.

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment