Kumekuwa na mjadala kuhusu sababu za kufa kwa Azmio la Arusha.
Azimio hilo lilianzishwa na Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama cha Tanu
kikiwa na lengo la kutilia mkazo imani na siasa yake ya Ujamaa na
Kujitegemea.
Halmashauri hiyo iliyokutana mjini Arusha Januari
26 - 29, 1967, ilijadili maadili ya viongozi wa umma, Serikali na vyombo
vingine, pamoja na wanachama wa Tanu.
Katika maadili ya viongozi wa
umma, iliamuliwa kuwa kiongozi wa Tanu (baadaye CCM) au wa Serikali,
sharti awe ama mkulima au mfanyakazi na asishiriki katika jambo lolote
la kibepari au kikabaila.
Hata hivyo baada ya Mwalimu Julius Nyerere
aliyekuwa anasimamia maadili hayo kung’atuka madarakani, misimamo hiyo
ilianza kuyeyuka na kupigiliwa msumari wa mwisho huko Zanzibar.
Maamuzi ya Zanzibar
Mwaka 1991 Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ilikutana mjini Zanzibar na kufanya mabadiliko ya azimio hilo.
Akizungumza na wazee wa chama, viongozi wa Taifa,
mashirika ya umma na watu binafsi Februari 25, 1991 jijini Dar es
Salaam, aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM hicho na Rais Ally Hassan Mwinyi
aliwatoa hofu wale wanaodhani kuwa azio la Arusha linageuzwa.
“Inaelekea
kuna hofu kwamba Azimio la Arusha linageuzwa. Kwa hiyo tangu mwanzo,
kabla ya kusema lolote, nataka tuelewane kwamba siasa yetu bado ni ile
ile ya Ujamaa na Kujitegemea,” anasema na kuongeza:
“Halikugeuka wala hatutazamamii kuligeuza. Kwa
hali yoyote sisi wanachama wa Chama cha Mapinduzi hatutaweza kuigeuza
siasa hii. Kule Zanzibar tulizungumza mengi, miongoni mwao ni kutoa
tafsiri ya baadhi ya vipengele vya Azimio ili vifanane na wakati
tulionao.”
Akifafanua zaidi, Mwinyi anasema tangu azimio hilo
lilipoanzishwa mwaka 1967 hadi mwaka 1991 ilikuwa imepita zaidi ya
miaka 20, hivyo kulikuwa na mabadiliko mengi duniani.
“Hali yetu ya
sasa hasa ya kiuchumi, siyo ile ya mwaka 1967. Ndiyo maana mishahara ya
wafanyakazi ingawa imeongezeka sana, lakini bado haikidhi mahitaji yao,
haiwatoshi hata wale wanaopokea mishahara mikubwa miongoni mwetu,”
anasema na kuongeza:
“Isitoshe, wakati wa Azimio idadi ya Watanzania
ilikuwa ndogo, sasa hivi idadi yetu imeongezeka zaidi ya mara mbili .
Kwa sababu ya wingi wetu, mahitaji yameongezeka sana, wakati mapato yetu
yamekuwa yakipungua wakati wote.”
Mwinyi anaongeza kuwa kila zama na mwongozo wake:
“Msahafu wa Waislamu unasema “Likulli ajalin kitab’, yaani kila zama ina kitabu chake,” anasema na kuongeza:
“Sisi
wana CCM tunakubali kuwa kila zama zinahitaji kuwa na mwongozo wake.
Azimio la Arusha ni mwongozo wetu wa msingi. Ni dira inayoongoza
mwelekeo wa jamii yetu. Lakini tafsiri zake inabidi zirekebishwe kila
inapohitajika ili zisipitwe na wakati.”
Akisisitiza kuhusu ufafanuzi wa maamuzi ya
Zanzibar anasema baada ya kutangazwa kwa azimio la Arusha mwaka 1967
lilifuatiwa na matamko kama vile Azimio la Iringa la mwaka 1971 la
‘Siasa ni Kilimo’ na mwongozo wa mwaka 1981 uliotolewa kwa lengo la
kukuza tafsiri ya Azimio la Arusha.
Anaongeza kuwa hata mwaka 1974 kulikuwa na agizo la Musoma kuhusu Elimu ya Kujitegemea.
“Maandiko
hayo yote hayakupingana na Azimio la Arusha, ila yaliongeza mambo
ambayo yalihitajika yafanane na wakati wake,” anasema.
Akizungumzia
sababu ya kuanzishwa kwa Azimio la Arusha mara baada ya nchi kupata
uhuru, anasema baadhi ya viongozi walianza kutumia uongozi wao kama
mradi wa kujineemesha.
Msimamo wa Nyerere
Licha ya
Rais wa awamu ya pili kufafanua umuhimu wa uamuzi wa Zanzibar, bado
Mwalimu Nyerere aliendelea kutoridhika kuhusu msimamo mpya wa CCM.
Akizungumza na waandishi wa habari mwaka 1999,
Mwalimu Nyerere alisema bado alikuwa hajaona kasoro ya Azimio la Arusha.
“Mimi bado natembea nalo (Azimio la Arusha). Nalisoma tena na tena
kugundua kama kuna cha kubadili. Labda ningeboresha Kiswahili
nilichokitumia, lakini Azimio lenyewe bado ni thabiti. Nisingebadili
hata neno moja,” anasema Mwalimu Nyerere.
Source:Mwananchi