Saturday, July 27, 2013

Majirani walonga kuhusu kiwanda cha bunduki Dar

Mtuhumiwa aliyekamatwa na polisi Julai 18 kwa tuhuma za kumiliki kiwanda cha silaha nyumbani kwake maeneo ya Kawe Mzimuni alifahamika na majirani zake kama fundi funguo.
Juzi, Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam ilitangaza kumshikilia mtu mmoja kwa tuhuma za kumiliki kiwanda cha kutengeneza silaha nyumbani kwake kinyume na sheria.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa kanda  hiyo,  Ally Mlege alisema  taarifa za uwapo wa kiwanda hicho walizipata baada ya kukamtwa kwa watuhumiwa wanne wa ujambazi.
Wakizungumza kwa masharti ya kutokutaja majina,  majirani hao walisema kijana huyo alikuwa akiishi katika nyumba ya familia pamoja na wazazi na  mkewe, na  alizoeleka mtaani kwa  jina la Makufuli na watu wengi walijua kutengeneza funguo ndio kazi yake iliyokuwa ikimpatia kipato.
Walisema alikuwa ni kijana wa kawaida na alikuwa akijumuika na vijana wengine wa mtaani kama kawaida na hawakuwahi kufikiria wala kuhisi alikuwa akijihusisha na biashara yoyote haramu katika nyumba hiyo ikiwamo  kumiliki  vifaa vya kutengenezea silaha kama SMG na Shotgun, zaidi ya ile ya ufugaji wa ngo’mbe  inayofanywa na familia hiyo
Wakielezea kukamatwa kwake mmoja wa majirani hao, alisema siku ya tukio majira ya saa sita mchana  waliona magari yakienda katika nyumba hiyo inayotazamana na Shule ya Msingi Kawe A na baadaye kuzuka purukushani zilizodumu kwa takribani  muda wa saa mbili.
Walisema baadaye  mtuhumiwa pamoja na mkewe walikamatwa kwa tuhuma hizo.
Walisema mtaa umekuwa kimya toka kutokee kwa tukio hilo kila mmoja akijaribu kutathimi ni kwa namna gani mtuhumiwa huyo aliweza kufanya biashara hiyo kwa siri ikiwa nyumba hiyo iko katika eneo la msongamano wa watu na pia karibu na uwanja ambao wanajeshi huwa wanafanyia mazoezi.
Jana nyumba aliyokuwa akiiishi mtuhumiwa  ilionekana kuwa kimya huku  mlango wa mbele ukiwa umefungwa, na nje kukiwa na zizi la ng’ombe.
Nyumba za jirani watu walioneka nje wakifanya shughuli zao kama kawaida,lakini wengi wao wakiwa makini kuongea .
Siku ya Jumanne Polisi Kanda maalumu ya Dar es Salaam ilitangaza kumshikilia mtu mmoja kwa tuhuma za kumiliki kiwanda cha kutengeneza silaha nyumbani kwake kinyume na sheria.
Kaimu kamanda wa polisi wa kanda Maalumu ya Dar es Salaam Ally Mlege alisema  taarifa za kuwapo kiwanda hicho walizipa baada ya kukamtwa kwa watuhumiwa wanne wa ujambazi.

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment