Saturday, February 23, 2013

Mfuko wa Bima ya afya wafananishwa na wizi

WANACHAMA wa Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) wa mkoani Simiyu, wilaya ya Meatu wamesema mfuko huo pamoja na kutokuwa na tija kwao ni sawa mnyanganyi anayewanyang’anya sehemu ya mishahara yao kwa njia ya udanganyifu.
Wakazi wa maeneo mbalimbali ya wilayani humo, wanaeleza kusikitishwa kwao na kitendo cha kukatwa mishahara yao mara tu wanapoajiriwa, kwa maelezo kuwa wanakuwa wamejiunga na NHIF bila hata kuhojiwa ikiwa wapo tayari kujiunga na mfuko huo au la.
Tatizo kubwa zaidi linaelezwa kuwa ni kukatwa fedha hizo zinazoelezwa kutumika kugharamia huduma za matibabu ya mwajiriwa na wanafamilia wake wasiozidi wanne, lakini imebainishwa kuwa wahusika hawapati huduma hizo kutokana na kutokuwa na kadi za uanachama na hivyo, mbali na kukatwa mishahara bado hujikuta wakitoa fedha taslimu kugharamia huduma hizo pindi wanapougua.
Paul Nlimandago (42) mkazi wa Majengo alisema mshahara wake ulikuwa ukikatwa michango ya mfuko huo kwa kipindi cha miaka minne huku yeye na familia yake wakipata huduma za afya kwa kulipa fedha taslimu, kutokana na kutopatiwa kadi za uachama.
“Nilipata kadi ya uanachama miaka minne tangu mshahara wangu ulipoanza kukatwa michango ya uanachama…, nilikuwa najaza fomu, napeleka picha na fedha zinakatwa kila mwezi kwa kipindi chote hicho  bila kupata kadi,” anabainisha Nlimandago
Naye Juma Said (43) anabainisha kuwa wanachama hawana imani na mfumo unaotumika kulipia gharama wanazotumia, kwani hutakiwa kuweka sahihi ambazo hazioneshi kiasi cha fedha kitakachodaiwa na watoa huduma, kwa ajili ya malipo ya huduma.
“Bima ya afya  ni wizi mtupu, mtu unatibiwa kisha unapewa makaratasi usaini huku gharama unazodaiwa kutokana na huduma uliyopatiwa zikiwa hazioneshwi; hii siyo sawa, nashauri fomu ambazo wanachama tunasaini baada ya kuhudumiwa zirekebishwe, iwekwe sehemu ambayo mtu utaona deni lako ili uidhinishe malipo unayoafiki kuyatumia,” Said anaeleza na kushauri.
Anasema jambo la kusikitisha zaidi ni mtu kutakiwa kusaini karatasi ambayo haufahamu wataenda kudai kiasi gani cha fedha kisha unaelezwa, “dawa ulizoandikiwa zote hazipo, nenda ukanunue nje.” anasema inaumiza na kukatisha tamaa kuliko maana inayopatikana katika neno sana.
Shaban Alley (40) anashauri mamlaka husika zifuatilie kwa karibu huduma wanazopatiwa wanaochangia malipo ya huduma za afya, kwa kufanya uchunguzi wa kushtukiza na kwamba wanaotakiwa kutekeleza jukumu hilo ni wasioishi eneo linalochunguzwa, ili kuondoa uwezekano wa kufichiana dhambi na kulindana.
“Wakitaka wapate ukweli, wanatakiwa  wafike ghafla bila kutoa taarifa na kujifanya wagonjwa wenye kadi za kuchangia huduma za afya kupitia NHIF au CHF, wakihitaji kuhudumiwa hata kwenye hospitali binafsi ambazo zina mikataba na NHIF; watashuhudia jinsi wanachama wao wanavyopata shida mbalimbali wanapohitaji huduma hizo,” anaeleza Alley
Greyson Kakulu, mwanachama mwingine wa NHIF anapotakiwa kuzungumzi hali ya huduma za afya akiwa katika mpango huo wa kulipia huduma za afya kabla ya kuugua anasema: “Siridhishwi hata kidogo ni mwaka wa tatu sasa tangu nijiunge na mfuko huu, kila mwezi mshahara wangu unakatwa lakini sihudumiwi kama mwananchama kwa sababu sina kadi,”anaeleza na kuongeza:
“Nagharamia huduma za afya ninazopatiwa mimi na familia yangu lakini ninapokwenda kudai kurejeshewa fedha zangu sijawahi kurudishiwa; hali hii inaumiza sana, hasa ikizingatiwa mtu huwezi kukataa kujiunga wala kujitoa, naomba ishughulikiwe.”

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment