Saturday, February 23, 2013

Kanisa katoliki laruhusu tembe za kuzuia mimba



Kanisa Katoliki nchini Ujerumani limeamua kuwa ni halali kwa mwanamke kutumia tembe ya kuzuia mimba mara tu baada ya kubakwa.
Uamuzi huu umefanywa kufuatia mkutano wa viongozi wa Kanisa Katoliki nchini Ujerumani baada ya mwanamke mmoja aliyekuwa amebakwa kusema kuwa alizuiwa kufanyiwa matibabu siku mbili mfululizo katika Hospitali zinazofadhiliwa na Kanisa Katoloki zikisema kuwa kuzima mimba ni kinyume cha maongozi yake.
Maaskofu nchini Ujerumani wamekuwa wakijikuta njia panda, ambapo upande mmoja wanahangaishwa na msimamo wa Kanisa Katoliki, na kwa upande mwingine tatizo lililompata mwanamke huyo aliyebakwa, kufukuzwa na hospitali zinazosimamiwa na Kanisa hilo zilizoko mjini Cologne.
Mwishowe Maaskofu hao walikubaliana kuwa itakuwa halali ikiwa tembe hizo zitatumiwa na mwanamke aliyebakwa kwa lengo la kuzuia kushika mimba badala ya kutoa mimba
Hii ina maana kuwa itaweza kutumiwa tu kama kifaa cha kuzuia kushika mimba lakini sio kuavya. Tembe hizo hutumiwa na wanawake wengi wasiotaka kushika mimba baada ya tendo la ndoa.
Hata hivyo Kanisa Katoliki nchini Ujerumani, ambako Papa wa sasa alitoka, limegawanyika kufuatia tendo hilo la ubakaji.
Ubishi kama huo nchini Marekani haukufikia uamuzi baada ya pande zote zilizokuwa zikibishania dawa hiyo kusema kuwa ni vigumu kujua kama baada ya kitendo cha ndoa asubuhi inayofuata mwanamke ameshika mimba au la.

No comments:

Post a Comment