Thursday, February 7, 2013

CHADEMA WAKAMILISHA MIKAKATI JUU YA SPIKA

WAKATI wabunge wa Chadema kutwa nzima ya jana wakiwa katika kikao kujadili hoja ya kuwasilisha katika kikao cha Bunge cha kutaka Spika aondolewe, kamati imeundwa kuchunguza mitalaa ya elimu ya Serikali.

Bunge limeunda Kamati ya Kuchunguza Mitalaa ya Elimu kutokana na hoja binafsi ya Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia, ambaye alidai mapema kuwa Serikali haina mitalaa ya elimu.

Nao wabunge wa Chadema wanataka kuondolewa kwa Spika na Naibu wake kwa sababu mbalimbali ikiwamo madai ya kutowatendea haki pamoja na kukalia rufani zao.
Akizungumza katika Viwanja vya Bunge mjini Dodoma, Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisema kuwa wamekamilisha mchakato wa taarifa yao ya kutaka Spika na naibu wake waondolewe na wataiwasilisha katika kikao cha Bunge wakati wowote kuanzia jana jioni.

“Tumeazimia kwa kauli moja, tunataka kumwengua spika pamoja na msaidizi wake kwa kuwa amekuwa akiminya haki, anakalia hoja pamoja na rufani,” alisema Lissu ambaye juzi akiwa bungeni aliomba mwongozo na kumlalamikia Spika Anne Makinda kuhusu kukalia hoja zao.

Rufani zinazolalamikiwa
Rufani ambazo Chadema wanazilalamikia kukaliwa ni pamoja na malalamiko ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika juu ya uamuzi wa Ndugai kwa kupeleka kwenye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ushahidi wa awali uliotakiwa kuwasilishwa na Mwenyekiti wa Bunge kuhusiana na tuhuma za Mwigulu Nchemba.

Rufani nyingine inayolalamikiwa na wabunge wa chama hicho, Spika kutotoa nafasi ya kujadiliwa suala la kutekwa kwa Dk Steven Ulimboka.

Hoja nyingine ambayo inadaiwa kutokufanyiwa kazi ni malalamiko dhidi ya uamuzi wa Spika kuhusu swali la Tundu Lissu kuhusu mauaji ya yaliyofanywa na polisi katika maeneo ya mgodi wa dhahabu wa Nyamongo, Wilayani Tarime mkoani Mara.

Hoja nyingine ni kutakiwa maelezo ya uthibitisho ya Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema juu ya kauli ya uongo ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika kikao cha tatu cha mkutano wa pili wa Bunge, Februari 10, 2011.
Pia kukaliwa kwa taarifa ya hoja ya kusudio la kuwasilisha hoja ya jambo linalohusu haki za Bunge.

Ndugai aunda tume
Hoja binafsi iliyowasilishwa mwishoni mwa wiki na James Mbatia kuhusu kuitaka Serikali iwasilishe bungeni mitalaa ya kufundishia, imeihenyesha Serikali na jana Ndugai alitangaza kuunda tume ya wabunge sita kwa ajili ya kuithibitisha mitalaa hiyo iliyowasilishwa bungeni na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa.

Aliwatangaza wajumbe walioteuliwa kuwa ni Mbunge wa Viti Maalumu , Magareth Sitta ambaye ndiye atakayekuwa Mwenyekiti, Abdul Marombwa, Khalifa Khalifa, Israel Natse, Yahaya Kassim na Benadeta Mshashu.

Wengine ni wataalamu kutoka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi pamoja na Waziri mwenye dhamana katika Wizara hiyo.

Wakati Mbatia akiwasilisha hoja yake aliapa mbele ya Bunge kuwa kama Serikali itawasilisha mitalaa hiyo, atakuwa tayari kujiuzulu nafasi ya ubunge kutokana na kile alichoeleza kuwa alikuwa na uhakika kwa asilimia zote kuwa hakuna mitalaa.

Lissu kusimamishwa
Naibu Spika, Ndugai amesema huenda Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akakumbana na rungu la Kanuni za Bunge kwa kusimamishwa miezi sita kuhudhuria vikao vya Bunge, endapo Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge itambaini moja kwa moja kuwa ndiye chanzo cha vurugu ndani ya Bunge.

Juzi, wakati akiahirisha kikao cha Bunge, Spika Makinda, aliliambia Bunge kuwa Tundu Lissu ndiye kinara wa vurugu zinazofanyika katika vikao vya Bunge. “Tundu Lissu, wewe ndiyo kinara wa vurugu humu ndani.”

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment