Friday, January 18, 2013

HIZI NDIZO SALAMU ZA LOWASA KWA WATANZANIA MWAKA MPYA.

Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, ameuanza Mwaka Mpya wa 2013 kwa kuwataka Watanzania kufanya maamuzi magumu kwenye kila changamoto itakayojitokeza mbele yao.

Katika sherehe ya Mwaka Mpya aliyoiandaa nyumbani kwake Monduli jana, Lowassa alisema kuwa ni muhimu kwa Watanzania kufanya maamuzi magumu katika kila changamoto watakazokabiliana nazo mwaka huu badala ya kubaki wakilalamika.

“Salamu zangu za mwaka mpya wa 2013 kwa Watanzania, nawaomba tuache kulalamika badala yake tufanye maamuzi magumu kwenye kila changamoto tutakazokabiliana nazo,” alisema Lowassa.

Mbele ya baadhi ya wabunge, viongozi wa CCM mkoa na wilaya nchini, Lowassa alisema katika kukabiliana na umaskini lazima kuongeza juhudi katika kufanya kazi kwani anaamini Watanzania wakiamua, inawezekana.

Lowassa alitumia hafla hiyo kukanusha taarifa za baadhi ya vyombo vya habari na kwenye mitandao ya kijamii kwamba hafla hiyo ilikuwa ya kisiasa.

“Wameandika katika mitandao ya kijamii kuwa kuna sherehe kubwa ya kisiasa nyumbani kwangu. Huo ni uzushi tu.

Nawaambia waache porojo hizo. Mimi nimekuwa nikiandaa sherehe hizo toka mwaka 1995, wao wakitaka waige mfano huu,” alisema Lowassa ambaye anatajwa kutaka kuwania urais mwaka. 2015.

Hii ni mara ya pili kwa Lowassa kuzungumzia suala la kufanya maamuzi magumu.

Mara ya kwanza alitoa kauli hiyo bungeni ambapo aliitaka serikali kufanya maamuzi magumu katika kutatua kero za wananchi.

Kauli hiyo iliibua mjadala mzito ndani na nje ya Bunge na hata ndani ya chama chake, huku baadhi wakienda mbali kwa kuhoji maamuzi magumu aliyopata kuyafanya alipokuwa Waziri Mkuu.

Baadhi ya viongozi waliohudhuria hafla hiyo ni pamoja na baadhi ya wabunge, wenyeviti na viongozi wengine mbalimbali wa mikoa na wilaya nchini.

Baadhi ya wabunge hao ni pamoja na Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo, Andrew Chenge (Bariadi Mashariki) na Peter Selukamba (Kigoma Mjini).

Wenyeviti wa mikoa walioshuhudia hafla hiyo ni Khamis Mgeja (Shinyanga), Dk. Walid Kabourou (Kigoma) na mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) toka Shinyanga, Salum Mbuzi.


No comments:

Post a Comment