Wednesday, January 23, 2013

Wapoteza maisha baada ya magari kuvaana uso kwa uso

WATU wawili wamefariki dunia baada ya magari mawili likiwamo la Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa) kugongana uso kwa uso juzi usiku katika Barabara kuu ya Moshi-Himo.
Ajali hiyo ilitokea saa 2:00 usiku katika Kijiji cha Miwaleni Kata ya Kirua Vunjo, Wilaya ya Moshi Vijijini baada ya gari la Kinapa Toyota Landcruicer kugongana na Toyota Corolla.
Dereva wa Toyota Corolla ambaye ni Fundi Makanika, Arcard Eligi alifariki dunia akipatiwa matibabu Hospitali ya Rufaa ya KCMC wakati abiria katika gari la Kinapa, Ally Mohamed alikufa papo hapo.
Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz alilithibitishia gazeti hili kuwapo kwa ajali hiyo lakini akasema hakuwa na taarifa kamili kwa kuwa alikuwa safarini kikazi mkoani Tanga.
Hata hivyo Mkuu wa Hifadhi ya Kilimanjaro (Kinapa), Erastus Lufungilo aliliambia gazeti hili kuwa abiria aliyekuwa katika gari la Hifadhi na kufariki dunia hakuwa mwajiriwa wa Kinapa.
“Ni ajali mbaya sana kwa sababu ukiangalia yale magari yalivyoisha (kuharibika) unaweza kupata picha hiyo, kishindo cha hiyo ajali ilikuwaje kwa kweli ni ajali mbaya,” alisema Lufungilo.
Lufungilo alisema dereva wa gari hilo la hifadhi pamoja na abiria katika gari dogo la binafsi lililogongana na gari la hifadhi, Harson Macha wote wamelazwa katika Hospitali ya Rufaa KCMC.
Polisi wanachunguza chanzo cha ajali hiyo iliyotokea juzi saa 2:00 usiku.

Source:Mwananchi

No comments:

Post a Comment