Friday, January 11, 2013

Lissu: Hakuna sababu ya baadhi ya watu kuwa juu ya sheria


MCHAKATO wa ukusanyaji wa maoni ya wananchi yatakayosaidia katika uundwaji wa Katiba Mpya unaendelea na safari hii ni zamu ya makundi maalumu vikiwemo vyama vya siasa ambavyo vimeanza kutoa maoni yao mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Mikutano hiyo kati ya Tume na wawakilishi wa vyama vya siasa inafanyika katika Ofisi Kuu za Tume pamoja na Ukumbi wa Karimjee Jijini Dar es Salaam.
Vyama vyote vimepewa fursa ya  kushiriki katika utoaji maoni na baadhi ya mambo ambayo wameyapendekeza kuwamo katika Katiba Mpya ni pamoja na utawala wa majimbo na kuwapo kwa mgombea binafsi.
Kimsingi hoja hizi zimekuwa zikitolewa maoni mara nyingi na wananchi katika mikutano mbalimbali ya Tume iliyokuwa ikifanyika nchi nzima kuanzia Julai hadi Desemba mwaka jana, tofauti na sasa ni kwamba wanasiasa wamezieleza kwa undani zaidi na kuzifafanua namna gani zinavyoweza kuingia katika Katiba ijayo.
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimejikita zaidi katika muundo wa Muungano na utawala wa majimbo, wakati Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimejielekeza kwenye hoja ya mgombea binafsi.
Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu anasema kuwa chama chake kinataka kuona Katiba Mpya inakuja na mfumo mpya ambao utaleta mabadiliko katika nyanja mbalimbali zikiwamo utawala, rasilimali, ulinzi wa mali za umma, haki za binadamu, uwajibikaji serikalini na muundo wa Jamhuri ya Muungano ambao utasaidia kuunusuru usivunjike.
Lissu anasema kuwa kuna kila sababu ya Katiba Mpya kuleta mabadiliko katika muundo wa Muungano ambao Chadema wanapendekeza uwe Muungano wa Shirikisho wa Serikali tatu, yaani Serikali ya Jamhuri ya Tanganyika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ndogo ya Jamhuri ya Muungano.
“Hatuwezi kuendelea na mfumo uliopo wa Muungano kwani una upungufu mwingi. Ni fursa nzuri ambayo tumeipata ya kutengeneza Katiba Mpya ya nchi ambayo kimsingi inapaswa kuleta mabadiliko yatakayounusuru au kuuokoa Muungano usivunjike. Tukikosea tunaweza kujikuta tunatengana kama ilivyo kwa Ethiopia na Eritrea, Sudan na Sudan Kusini, Yugoslavia na Czechoslovakia,” anasema Lissu.
Pia anasema kwa kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni wa hiari kunatakiwa kuwe na haki ya kujitoa kwa upande usioridhika kuendelea kuwa kwenye Muungano.
Anasema utaratibu wa kujitoa uwe kwa njia ya kura ya maoni itakayopigwa na wananchi wa upande mmojawapo wa Muungano na ikiwa theluthi mbili ya wananchi wakikubali kujitoa basi iruhusiwe wajitoe kwa sababu Muungano huu haukuwa wa lazima.
Lissu anaongeza kuwa kwenye mambo ya Muungano wamependekeza yawemo mambo saba tu ambayo ni ulinzi na usalama, wizara zisizozidi 18, Bunge lisilozidi wawakilishi 300, mamlaka ya uteuzi ya Rais ambayo yanapaswa kupunguzwa, Rais ashtakiwe akifanya makosa ya jinai, pamoja na kuweka bayana suala la umilikaji wa rasilimali za nchi.
Kuhusu mamlaka ya uteuzi ya Rais anaeleza kuwa ni lazima yapunguzwe ili kuiondoa nchi kwenye mfumo wa urais wa kifalme.

No comments:

Post a Comment