Saturday, December 29, 2012

UFARANSA YAKATAA OMBI



Ufaransa imekataa ombi la rais wa Jamhuri ya Afrika ya Kati Francois Bozize kusaidia kuwarudisha nyuma waasi wanaotishia kuiangusha serikali yake, huku Marekani ikiamua kufunga ubalozi wake nchini humo.
Wasiwasi umezidi kutanda nchini humo wakati muungano wa waasi hao unaojulikana kama Seleka ukizidi kusonga mbele kuelekea mji mkuu Bangui, kwa madai kuwa serikali imekiuka makubaliano ya amani yaliyosainiwa mwaka 2007. Lakini rais Francois Hollande wa Ufaransa amekataa ombi la rais Francois Bozize akisema kuwa muda wa kufanya hivyo ulikwisha.
Wakati huohuo,Marekani kwa upande wake imetangaza jana Alhamisi kuwa inasitisha shughuli zote katika ubalozi wake mjini Bangui, na kwamba balozi wake na wafanyakazi wengine wa ubalozi huo walikuwa wameondoka nchini humo. Msemaji wa wizara ya mambo ya kigeni ya Marekani, Patrick Ventrell, alisema uamuzi huo ulichukuliwa kwa kuhofia usalama wa wafanyakazi hao, na kwamba hatua hiyo haihusiani kwa namna yoyote ile na uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia baina ya mataifa hayo mawili. Marekani pia iliwatahadharisha raia wake dhidi ya kusafiri kwenda Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Hayo yanajiri wakati viongozi wa kanda hiyo wakijaribu kuratibu makubaliano ya kusitisha mapigano na waasi walikuwa wamesema wamesimamisha kwa muda, operesheni kuelekea mji mkuu, ili kuruhusu mazungumzo kufanyika. Waasi hao wanataka serikali itekeleze makubaliano ya kuwatawanya na kuwaingiza katika maisha ya kiraia.
"Wapiganaji wanataka pesa walizoahidiwa ili kuweza kujiunga na jamii ya kiraia, programu ya kuwatawanya ilihusu kuwanyang'anya silaha wapiganaji lakini yote hayo hayakutekelezwa na ndiyo matatizo makubwa. Lingine ni kuundwa kwa ajira kwa waasi kwa lengo la kuwaingiza katika maisha ya kiraia," alisema Thierry Vircoulon kutoka shirika la kutatua migogoro la International Crisis Group, anafafanua madai ya waasi hao.

No comments:

Post a Comment